Chuo Kikuu cha Yale na Sheng
Juzi nilijiunga na wasomi wengine kutoka pembe zote za dunia katika chuo maarufu cha Yale kujadili mambo yanayohusu mabadiliko ya lugha katika miji barani Afrika. Chuo kikuu kiligharamia usafairi na mahitaji mengine na wasomi waliwasilisha utafiti wao. Wasomi walitoka Afrika, Ulaya, na Marekani.
Nilifurahi sana kupata fursa ya kubadilishana mawazo ya kiisimu na watafiti wanaotafiti lugha kama Sheng ya Nairobi, Tsotsitaal ya Soweto, Kindubile ya Kongo, Iscamtho ya Afrika Kusini, KiNaija cha Nigeria, Kiswahili kinachoiga Kizungu nchini Tanzania, na kadhalika.
Kwenye mazungumzo na msomi kutoka Lubumbashi, Kongo nilijifunza tofauti kadha za Kiswahili chao na Kiswahili sanifu.
Jumatatu inaitwa 'kazi moja,' Jumanne 'kazi mbili,' Jumatano 'kazi tatu,' Alhamisi 'kazi nne,' Ijumaa 'kazi tano,' halafu Jumamosi ni 'POSHO.' Nikashangaa kwa nini lakini nikaelezwa kuwa walizihesabu siku kulingana ya kazi waliofanyishwa na wakoloni wabelgiji. Kutoka Jumatatu mpaka Ijumaa walifanya lakini siku ya Jumamosi walipata mshahara yaani posho.
'